DIMBWI LA HUBA SEHEMU YA 2



SIMULIZI: DIMBWI LA HUBA

MTUNZI: ALLY MBETU

SEHEMU YA PILI

Mama yake baada ya kumkosa mchana wakati wa chakula, baada ya kumuona

amerudi alimfuata kutaka kujua alikuwa wapi. Alipoingia chumbani alishtuka

hali aliyomkuta nayo mwanaye.

“Sued mwanangu mbona hivi! Unaumwa?”

“Hapana.”

“Sasa mbona upo hivyo?”

“Basi tu mama natamani kufa.”

“Kufa?”

“Ndiyo mama.”

“Kwa nini?”

“Nina imani bila Zulfa siwezi kuishi?”

“Zulfa ndiye nani?”

“Mwanamke niliyemchagua kuwa mke wangu.”

“Sasa huyu Zulfa kafanya nini?”

“Nimeambiwa anataka kwenda nje kusoma.”

“Sasa tatizo nini?”

“Sicho tulichokipanga, mzee wake ana roho mbaya aliona kumuoa mwanaye

ningefaidi.”

“Huyo Zulfa anakaa wapi?”

“Kayenzo.”

“Kayenzo, mtoto wa nani?”

“Kipepeo.”

“Yule tajiri wa Kayenzo?”

“Ndiyo mama.”

“Mwanangu mbona unataka mazito, kwanza baba yako akisikia unafikiri

kutakuwa na usalama? Unataka kumchokoza baba yako? Kwanza mapenzi

umeyaanza lini mpaka kufikia hatua ya kupanga na ndoa wakati huna kazi wala

chumba.”

“Ningejua nitamuweka wapi na anakula nini.”

“Mwanangu achana na wazo hilo, muda ukifika utampata msichana mwingine

mzuri kuliko Zulfa.”

“Mama hakuna mwanamke mwingine atakayempiku Zulfa, mama sikuwahi

kupenda na sitapenda tena zaidi ya Zulfa.”

“Basi ndiyo hivyo amekwenda kusoma na akirudi atatafuta msomi mwenzake

wewe wa kidato cha nne umeula wa chuya.”

“Mama wee fanya utani, mimi bila ya Zulfa siwezi kuishi.”

“Umekula?”

“Kuna faida gani ya kula wakati sina furaha.”

“Mwanangu kula, kila kitu niachie mimi.”

“Utafanya nini?”

“Mimi najua, kula kwanza.”

Sued alikubali kula huku akisubiri kujua mama yake anataka kufanya nini ili

kuweza kumpata Zulfa.

***

Upande wa pili, Zulfa wiki mbili kabla ya kurudi shuleni moyo wake ulikuwa

na shauku ya kumuona mpenzi wake Sued, kiumbe aliyeuteka moyo wake.

Wiki mbili kwake ilikuwa kama miaka ishirini, akiwa amekaa chumbani kwake

akicheza gemu kwenye laptop yake, mama yake alikwenda chumbani kwake

akiwa na uso wa furaha.

“Hodi mwanangu.”

“Karibu mama,” Zulfa aliacha kucheza gemu na kumtazama mama yake,

akakutana na uso uliojaa furaha.

“Mama mbona unaonekana una furaha?”

“Ni kweli mwanangu nina habari njema kwako.”

“Habari gani mama?”

“Ile nafasi aliyokuwa akiitafuta baba yako imepatikana.”

“Nafasi! Nafasi gani?”

“Ya kwenda kusoma nje.”

“Nje wapi?”

“Ina maana huna taarifa kuwa kuna nafasi ya kwenda Sweden?”

“Ndiyo najua.”

“Basi mwanangu baada ya miezi miwili na nusu unatakiwa uondoke kwenda

kuanza masomo.”

“Nitakwendaje wakati sijamaliza shule?” Zulfa alishangazwa na taarifa zile za

ghafla.

“Hiyo siyo sababu, elimu yako haihitaji kumaliza shule unaweza kujiunga tu.”

“Lakini mimi sikupanga kwenda sasa hivi.”

“Hiyo siyo juu yako, wewe ni mtoto tu unatakiwa kukubaliana na

kinachoamriwa na wazazi wako.”

“Sawa, lakini mimi naona hakuna umuhimu wa kwenda kusoma nje kwani

elimu ya sasa nchini imekuwa sana.”

“Acha ujinga huoni watoto wa vigogo wote wanasoma nje?”

“Mbona Wazungu wanakuja kusoma chuo kikuu huku?”

“Zulfa sitaki kuulizwa maswali ya kitoto, mi nilifikiri ungefurahi kusikia

umepata nafasi adimu ya kwenda kusoma nje! Nafasi yenyewe baba yako

kapoteza fedha nyingi ili kuhakikisha unaipata hasa baada ya kuonesha una

uwezo wa kielimu kuliko ndugu zako wote. Tena mimi mama yako ndiye

niliyekuwa nikimsumbua kila siku, hata sehemu aliyokata tamaa nilimpa moyo

na hatimaye imepatikana.”

“Lakini mama mimi sasa hivi siendi popote mpaka nimalize elimu yangu si

bado miezi sita tu?”

“Hiyo miezi sita ya kwako, lakini yetu unatakiwa uondoke haraka ili kuwahi

mwanzo wa masomo mapema.”

“Mama mi siendi.”

“Nini?” mama Zulfa alishtushwa na kauli ya mwanaye.

“Nasema siendi mpaka nimalize shule.”

“Zulfa unatania au unasema kweli?”

“Nasema kweli mama, siendi popote mpaka nimalize shule.”

“Zulfa hebu acha utani mama.”

“Mama nasema kweli wala sitanii, siendi popote mpaka nimalize shule, kama

mlijua hivyo hakukuwa na haja ya mimi kusoma mwaka huu.”

“Hayo unayosema utakuja kumueleza baba yako?”

“Nitamueleza tu mama.”

Mama Zulfa alitoka chumbani kwa binti yake huku akiwa amepoteza furaha

yake na kumshangaa mwanaye kugoma kwenda kusoma nje ya nchi na kutaka

kuendelea na elimu ambayo siku zote ilionekana ya kubabaisha japo kuna shule

za kulipia zilikuwa zikijitahidi kidogo.

Aliamini kinachomsumbua mwanaye ni hali ya mazoea, kuzoea mazingira ya

shule na mashoga zake. Lakini aliamini kama angemuelewesha faida ya kwenda

kusoma nje bila kutumia nguvu wala kulifikisha suala hilo kwa baba yake

angemuelewa.

Chumbani, Zulfa baada ya kutoka mama yake alijikuta akipoteza furaha ya

muda mfupi aliyokuwa nayo ya kuomba muda uende haraka ili aende kuonana

na mpenzi wake Sued. Taarifa ya mama yake iliivuruga furaha yake yote kwa

kumlazimisha kwenda kusoma nje.

Moyoni aliichukia safari ile ya kwenda kusoma nje, kitu alichokitaka mbele

yake ni penzi la Sued na si kingine kwa wakati ule. Aliapa kupigana kwa

nguvu zote ili amalize kipindi kile ndipo ajue atafanya nini.

Jioni mama yake kabla ya kufikisha ujumbe wa Zulfa kwa baba yake,

alimfuata tena chumbani kwake na kumbembeleza:

“Mwanangu Zulfa bado una msimamo wako?”

“Mama mimi siendi popote bila kumaliza muda wangu uliobakia.”

“Sikiliza mwanangu, hebu funguka mawazo. Safari hii ina faida kubwa sana

maishani mwako.”

“Sijakataa, ila mpaka nimalizie muhula wa mwisho. Nimejiandaa kwa ajili

ya kumaliza shule na mawazo yangu yote nimeyaelekeza huko na si nje ya

nchi.”

“Mwanangu hebu nielewe, hii ni nafasi adimu tena nimemlazimisha sana

baba yako, unafikiri atanielewaje?”

“Mwambie miezi sita siyo mingi avumilie nitakwenda.”

“Na masomo nayo yakusubiri?”

“Mlitakiwa mnieleze mapema, nimejifua kuhakikisha mtihani wa mwisho

napata ‘division one’, tena ya alama za juu.”

“Hiyo haina umuhimu kama elimu tuliyokutafutia.”

“Elimu ya hapa kwangu ina muhimu mkubwa, kuna watu tulipinga nani

atamzidi mwenzake, itaonekana nimewakimbia.”

“Hata wakisema, ukirudi utakuwa upo juu kuliko wao.”

“Sawa, lakini mimi siendi.”

“Kwa hiyo upo tayari nimwambie baba yako?”

“Nipo tayari.”

“Haya tusilaumiane.”

“Nitamwambia ukweli.”

Mama Zulfa aliona ushawishi wake umegonga mwamba kutokana na akili za kitoto za mwanaye. Aliamua kwenda kumwambia baba yake huenda akimkemea atabadili msimamo wake.

Mama Zulfa aliona ushawishi wake umegonga mwamba kutokana na akili

za kitoto za mwanaye. Aliamua kwenda kumwambia baba yake huenda

akimkemea atabadili msimamo wake.

Baba Zulfa aliamini ule ni utani wa mwanaye, alijua anamtania mama yake

hivyo hakuwa na wasiwasi na taarifa ile.

Majira ya saa nne usiku baada ya shughuli zote za kutwa, kula na kuoga,

mzee Kipepeo alimtuma msichana wa kazi kumfuata Zulfa aliyekuwa

chumbani amejilaza huku amefura kwa hasira kutokana na taarifa

alizoletewa na mama yake za kwenda kusoma nje ya nchi.

Zulfa alikuja mbele ya wazazi wake waliokuwa wamekaa sebuleni

wakiangalia vipindi vya usiku kwenye runinga. Alipofika, bila kusema kitu

alikaa kochi la karibu na wazazi wake. Mzee Kipepeo aliyaondoa macho

kwenye runinga na kumgeukia mwanaye aliyeonesha hayupo katika hali yake ya

kawaida.

“Zulfa mama,” alimwita kwa sauti ya chini yenye kusikika.

“Abee,” aliitikia kwa sauti ya chini bila kuwaangalia wazazi wake.

“Eti mama kuna nini?”

Zulfa hakujibu kitu, alitazama chini tu kitu kilichomfanya baba yake kumgeukia

mkewe na kumuuliza:

“Mke wangu ni hilihili tu au kuna lingine?”

“Ni hilo tu mume wangu kama kuna lingine aseme mwenyewe.”

“Eti mama hutaki kwenda kusoma nje?”

“Sijakataa ila mpaka nimalize muda wangu uliobakia.”

“Mwanangu elimu ya maana ni nje ya nchi hivyo nafasi hii ni ya dhahabu

mwanangu.”

“Baba nielewe, mimi nipo tayari kwenda kusoma nje lakini nina imani miezi

minne iliyobakia si mingi kwa nini nisimalizie nijue nimevuna nini?”

“Hayo hayana umuhimu tena, kama umepata nafasi hii ambayo tumegombea

watu wengi, tulikuwa watu zaidi ya mia moja, nafasi zilikuwa tano tu, tena watu

maarufu lakini uwezo wangu na nguvu yangu kubwa serikalini tumepata moja

kati ya nafasi hizo chache.”

“Wazazi wangu sijakataa, nimekubali ila baada ya kufanya mtihani wangu wa

mwisho.”

“Sikiliza, kuondoka kwako si ombi bali amri, umebakiwa na miezi miwili, shule

hutarudi tena zaidi ya kujiandaa na safari yako.”

“Kama amri mi siendi.”

“Nini?” baba yake aliuliza kwa sauti ya ukali.

“Nasema siendi popote,” Zulfa alijibu kwa kiburi.

“Kama huendi na hapa uondoke,” baba yake alimtisha.

“Sawa nitaondoka,” Zulfa alizidi kumjeuria baba yake.

“Wewe Zulfa jeuri ya kumjibu hivyo baba yako umeitoa wapi?” mama aliingilia

kati.

“Sijaitoa popote, kwa nini hamtaki kunisikiliza na mimi? Hata kama ni mtoto

nina haki ya kusikilizwa.”

“Sasa nasema hivi shule utakwenda kwa nguvu au kwa hiyari,” baba alitoa

amri.

“Kama mtanilazimisha nitakunywa sumu.”

“Kunywa tu.”

“Sawa, nitakunywa mfurahi.”

“Unajua wewe mtoto unataka kunichezea,” mzee Kipepeo alisema huku

akinyanyuka na kumfuata Zulfa aliyekuwa bado amekaa kwenye kochi. Alipofika

alimshika mkono na kumnyanyua, akamuuliza kwa hasira:

“Wee kinyago unasemaje?”

“Kama nilivyosema siendi mpaka nifanye mtihani wa mwisho,” Zulfa alijibu

kwa kujiamini.

“Etiii,” mzee Kipepeo alimsukuma kidogo mwanaye na kumpelekea kofi zito

lililomrusha nyuma na kujigonga ukutani, akateremka chini ya zulia.

“Pumbavu, wewe ni nani unayeweza kubishana na mimi?” mzee Kipepeo

alisema kwa hasira.

Lilikuwa ni kofi zito lililompata barabara Zulfa, akajigonga ukutani na kuanguka

chini akiwa amepoteza fahamu.

“Mume wangu umefanya nini?” mama Zulfa alishtuka baada ya kushtushwa

na muanguko wa mwanaye.

“Mpumbavu huyu, hawezi kunikosea heshima. Nimepoteza kiasi gani cha

fedha kwa ajili yake?”

“Lakini mume wangu hukutakiwa kuchukua uamuzi mzito kama huu, ona

mtoto ulivyomfanya.”

Mama Zulfa alisema huku akimtazama mwanaye aliyekuwa amepoteza

fahamu huku damu zikimtoka mdomoni na puani.

“Umeua mume wangu,” mama Zulfa alisema huku akilia.

“Nini?” Mzee Kipepeo alishtuka.

“Umemuua mtoto.”

“Nooo, hapana!”

Mzee Kipepeo alimbeba Zulfa na kutoka naye nje hadi kwenye gari na safari

ya kuelekea hospitali ikaanza mara moja, mkewe akiwa ametoka na nguo ya

kulalia, khanga aliyojifunga ilimdondoka bila mwenyewe kujua, hakukumbuka

hata kuvaa viatu.

****

Wakati nyumbani kwa mzee Kipepeo yakiendelea hayo, mjini Sued naye

alikuwa ameuwasha moto. Usiku baba yake baada ya kurudi alielezwa na

mkewe matatizo ya mwanaye. Baada ya kumsikiliza mkewe alitumwa mtu

kwenda kumwita. Sued aliyekuwa amevimba macho kwa kulia, alifika mbele ya

baba yake.

“Vipi wewe?”

Sued hakujibu kitu, alitazama chini baba yake alimuuliza tena.

“Una tatizo gani?”

“Sina,” alijibu kwa sauti ya chini.

“Eti na wewe umekua siku hizi?”

Sued hakujibu kitu, aliinama tu. Kitendo kile kilimuudhi sana baba yake,

akamsogelea na kumtikisa huku akimuuliza:

“Unalia nini?”

Sued bado hakujibu kitu, alihofia kumwambia baba yake yaliyo moyoni

mwake.

“Baba Sued si nimekueleza vituko vya mwanao?”

“Eti una mpenzi?”

Swali lilikuwa zito kwa Sued na kujikuta kwa mara nyingine akikosa jibu,

kitendo kile kilimuudhi baba yake. Kwa hasira alisema kwa sauti ya juu:

“Unasikia wewe ngedere, upuuzi wako sitaki kuusikia tena, haya toka mbele

yangu.”

Sued alirudi chumbani kwake huku akishukuru kutopigwa na baba yake

ambaye alikuwa mkali kama pilipili. Moyoni alijiapiza kuwa atamtafuta popote

mpenzi wake kabla hajaondoka. Japo alikuwa hajawahi kufika Kayenzo lakini

aliapa kuhakikisha anafika hata kuingia katika jumba la mzee Kipepeo ili tu

amuone mpenzi wake Zulfa.

Zulfa baada ya kufikishwa hospitali, alipatiwa huduma ya haraka na kuonesha

alipata mshtuko kichwani baada ya kujigonga ukutani. Alipewa mapumziko ya

siku moja kabla ya siku ya pili kuruhusiwa kurudi nyumbani huku msimamo

wake ukiwa uleule wa kuendelea kusoma na kufanya mtihani ndipo aende Ulaya

kusoma.

Wazazi wake hawakujua mtoto wao hakuwa na hamu ya kusoma kama

alivyosema zaidi ya kukutana na mpenzi wake Sued. Moyoni aliamini kabisa

alichokuwa akikikosa katika maisha yake kilikuwa ni kumpata mtu sahihi

atakayeupokea moyo wake kwa mikono miwili.

Sued alikuwa mwanaume wa kwanza kumteka kiakili, kimoyo na kimwili,

hakuwaza kumkosa kwa ghafla kiasi kile. Aliamini kama atakubali kwenda Ulaya

kusoma tena bila kumuaga lazima atamuona si mkweli na kutafuta mpenzi

mwingine.

Siku zote aliamini mapenzi ya kweli si fedha bali upendo wa dhati toka moyoni

mwa mtu, hata kama angekwenda kusoma nje na kurudi na madigrii mangapi

kama hakuonesha upendo wa dhati kwa Sued hawezi kumkubali na matokeo

yake kuangukia kwa wanaume wasio na mapenzi ya kweli.

Pamoja na umri wake wa miaka 19, alikuwa na ufahamu mkubwa katika

mapenzi. Aliogopa kumpa mtu asiye sahihi moyo wake na mwisho kuambulia

mateso mazito. Katika maisha yake, alipanga kumpa mtu dhamana ya moyo

wake ambaye atakuwa sahihi.

Cha ajabu, kwa nguvu za aina yake alijikuta akimkabidhi moyo wake Sued,

mvulana ambaye kwa muda mfupi moyo wake ulimuamini kwa asilimia kubwa

na kumuona ndiye chaguo sahihi kwake.

Cha ajabu, kwa nguvu za aina yake alijikuta akimkabidhi moyo wake Sued,

mvulana ambaye kwa muda mfupi moyo wake ulimuamini kwa asilimia kubwa

na kumuona ndiye chaguo sahihi kwake.

Kwa kipindi kifupi, alijikuta akitamani kuwa naye kiasi cha kutotamani tena

kuendelea na masomo zaidi baada ya mtihani wake wa kidato cha sita. Alijiona

tayari anafaa kujiamulia maisha yake, hasa katika mapenzi kwa vile alikuwa

tayari anajua zuri na baya pia kuwa na utashi wa kujiamulia kitu akipendacho.

Moyoni alipanga kupigana kwa nguvu zote kuhakikisha haendi nje kusoma

japo aliamini wazazi wake walikuwa na nguvu kubwa. Kwa muda uliokuwa

umebaki, alipanga kutoroka na kwenda mjini kumfuata Sued ambaye angejua

wafanye nini kwa kuamini angeondoka na kiasi kikubwa cha fedha ambacho

kingewawezesha kuishi sehemu yoyote chini.

Pamoja na kujua hasira za baba yake huku mama yake akijitahidi

kumbembeleza kubadili msimamo wake, lakini hakuwa tayari kumkubalia

mama yake ili wajue kweli amepania kumaliza mtihani wake wa kidato cha sita

uliokuwa umebakia miezi minne kufanyika.

***

Wazazi wake walizidi kumbembeleza aende shule kwa hiyari yake kuliko

kulazimishwa lakini bado Zulfa alishikilia msimamo wake. Baba yake alimueleza

atake asitake lazima atakwenda kusoma. Akaendelea kuwatishia wazazi wake

kuwa kama watamlazimisha basi atajiua. Tishio lile lilimtisha sana mama yake na

kutaka ushauri kwa mumewe kuliko kutumia nguvu nyingi.

“Sasa mume wangu tutafanya nini maana mtoto pamoja na vitisho vyote

bado msimamo wake upo palepale na sasa bado wiki mbili wakati kila kitu kipo

tayari kwa safari, itakuwaje?”

“Mke wangu ni utoto tu unamsumbua, akifika huko atatulia mwenyewe,

kwani wewe ulikuwa na wazo gani?”

“Wasiwasi wangu ni kumpoteza mtoto wetu, si unajua ndilo jicho letu.”

“Ni kweli lakini lazima wazazi tuoneshe msimamo ili mtoto asituendeshe.”

“Utakuwa umesababisha wewe.”

“Kwa nini mke wangu?”

“Ulimlea kama mtoto wa jicho kiasi cha kunikataza hata mimi mama yake

nisimfokee.”

“Lakini mke wangu kumtafutia shule nje kuna ubaya gani?”

“Hakuna ubaya lakini ndiyo hivyo na yeye alikuwa amepanga yake sasa

tutafanyaje?”

“Ile ni tisha toto tu, atatulia mwenyewe.”

Wakiwa katikati ya mazungumzo, Zulfa alitokea na mabegi yake, kitu

kilichowashangaza wazazi wake.

“Wee mtoto unakwenda wapi?” mama aliuliza.

“Shule,” aliwajibu kwa mkato.

“Kufanya nini?” baba mtu aliuliza.

“Kusoma.”

“Wee mtoto una wazimu, hebu rudisha mabegi yako ndani bado wiki mbili

uondoke.”

“Kwenda wapi?” Zulfa alijibu kwa kiburi, kitu kilichowashangaza wazazi wake

na kujiuliza jeuri ile kaitoa wapi.

“Mwanangu Zulfa una nini mama?” mama yake alimuuliza huku akimfuata

alipokuwa amesimama.

“Mama kwa nini hamtaki kunielewa?”

“Kukuelewa kivipi?”

“Nataka kurudi shule nikafanye mtihani japo nina imani nimepoteza vitu

vingi lakini kwa muda uliobakia lazima nitapata chochote, bado dhamira

yangu ya kupata ‘division one’ tena ya juu ipo palepale.”

“Tunajua lakini chonde mwanangu hebu badili msimamo wako kwani elimu

ya nje ni nzuri hata kukuwezesha kupata kazi nzuri popote katika dunia hii.”

“Ni kweli lakini kwanza nimalizie elimu niliyoisotea kwa miaka kumi na tatu,

nawashangaa nyie kwani bado miezi mitatu tu nimalize lakini hamtaki.”

“Sikiliza mwanangu, sisi wazazi wako hatuwezi kukupeleka sehemu

mbaya, tumepoteza fedha nyingi kuipata nafasi hiyo. Nakuomba mwanangu

kipenzi badili uamuzi wako ili uende kusoma,” mzee Kipepeo alimbembeleza

mwanaye.

“Si mnanilazimisha, basi mtapeleka mzoga wangu kwenda kusoma.”

Zulfa alisema huku akielekea chumbani kwake, kauli ile iliwafanya wazazi

wake kugeukiana na kutazamana, kila mmoja akitafuta jibu kwa mwenzake.

“Itakuwaje?” mama Zulfa alimuuliza mumewe.

“Yaani naushangaa ujasiri wa mwanao, sijui ameutoa wapi? Lakini utapoa

tu, bado utoto unamsumbua kwa vile hajui faida ya kile anachokifuata huko

nje.”

“Mume wangu unafanya utani mtoto yupo serious.”

“Sasa unataka tukubaliane na matakwa yake, mtoto siku zote ni kupata amri

ya wazazi wake.”

“Lakini kauli yake ya kupeleka mzoga wake umeichukuliaje?”

“Ni vitisho tu, kwenda nje ndiyo ajiue?”

Zulfa pamoja na vitisho vyote bado wazazi wake hasa baba yake msimamo

wake ulikuwa uleule wa yeye kwenda kusoma nje ya nchi. Aliamini akitumia

kiburi huenda akakosa kila kitu, akaamua kurudi matawi ya chini ili wazazi

wake waamini amekubali kwenda kusoma na yeye kupata nafasi ya kutoroka

kumfuata Sued mjini.

Alitoka chumbani na kuwafuata wazazi wake waliokuwa wamekaa sebuleni

wakiwa hawajui wafanye nini baada ya msimamo mkali wa mtoto wao,

kitu kilichowachanganya sana. Kama isingekuwa amelipa fedha nyingi basi

wangekubaliana na matakwa yake.

Wazazi wake walipomuona akisogea mbele yao bila mabegi, walinyamaza

na kumtazama mtoto wao anataka kusema nini. Zulfa alipofika mbele ya

wazazi wake alipiga magoti, kitu kilichowashangaza na kujiuliza kwa nini

anafanya vile.

“Baba,” alianza kumwita baba yake.

“Naam mwanangu,” baba yake aliitikia kwa shauku ya kutaka kujua mtoto

wake anataka kusema nini.

“Mama,” alimwita pia mama yake.

“Abee mwanangu.”

“Wazazi wangu naomba mnisamehe sana kwa yote niliyoyafanya kwa

kuwakosea heshima kwa kukataa mlichonitafutia. Naomba radhi sana wazazi

wangu kwa kuwakosea kwa kiasi kikubwa.”

“Tumekusamehe mtoto wetu, pia nilifurahi sana kusikia kauli yako na

kugundua kosa lako hakika umekuwa mwenzetu,” Mzee Kipepeo alisema akiwa

amejaa tabasamu pana.

“Hata mimi mwanangu sijawahi kupata furaha ya ajabu kama leo yaani

nimefarijika sana kama siku niliyojifungua na kukuleta duniani, asante

sana mwanangu kwa kutambua thamani yetu kwako,” mama Zulfa alisema

akimkumbatia mwanaye huku machozi yakimtoka.

“Wazazi wangu najua kiasi gani nimewavunjia heshima, najua kiasi gani

uamuzi wangu ulivyowachanganya. Kuanzia sasa hivi wazazi wangu nimekubali

kwenda kusoma nje ya nchi.”

“Asante mwanangu kwa kukubaliana nami,” mzee Kipepeo alimkumbatia

mwanaye aliyeanza kumnyima raha.

“Basi wazazi wangu naomba nikapumzike.”

“Hakuna tatizo mama kapumzike.”

Zulfa alirudi chumbani kwake akiwa na furaha baada ya mpango wake kwenda

kama alivyotaka kwa kuwapumbaza akili wazazi wake ili wiki mbili zilizobaki

aweze kujipanga na kutoroka.

Baada ya kuondoka, wazazi wake walikuwa na furaha sana, mzee Kipepeo

akamwambia mkewe:

“Unaona eeh! Tungelegeza angetupanda kichwani.”

“Siamini yaani mwanangu leo kanifurahisha sana.”

“Wacha nifike mjini mara moja, Zulfa leo alinichanganya sana.”

Mzee Kipepeo alitoka nje kwa ajili ya kwenda mjini na kumwacha mkewe

akiwahimiza wafanyakazi waandae chakula cha mchana.

***

Sued baada ya uzalendo kumshinda aliamua kwenda Kayenzo kumtafuta Zulfa

kabla ya muda wake wa kusafiri. Alipanda malori hadi njia panda ya kuelekea

Kayenzo, haukupita muda mrefu ilipita ‘pick up’ inayoelekea Kayenzo aliomba

lifti na kukubaliwa.

Alifika katika Mji wa Kayenzo majira ya saa tano asubuhi, mji ule alikuwa

mgeni hivyo hakujua mzee Kipepeo anakaa sehemu gani. Alimuuliza kijana

mmoja aliyekuwa akiuza karanga.

“Samahani, eti mzee Kipepeo anakaa sehemu gani?”

“Fuata hii barabara kuelekea ziwani, ukifika tu utakuta jumba la kifahari ndipo

hapo kwa mzee Kipepeo.”

“Asante.”

“Tena mzee Kipepeo huyo anapita.”

Sued alimtazama yule mzee aliyekuwa kwenye gari la kifahari, kisha

alimshukuru yule kijana. Alifuata barabara ya kuelekea ziwani kwa mwendo wa

dakika kama saba na kujikuta akitokea kwenye jumba kubwa lililokuwa na uzio

mkubwa.

Alisimama na kujiuliza atafanyaje ili kuwasiliana na mpenzi wake, alijitahidi

kuuzunguka ule uzio labda atamuona Zulfa au hata mfanyakazi wa pale ili

amuagize. Kwa mbali alimuona mfanyakazi akikatia majani alimwita kwa

kumfanyia:

“Psiiiii.”

Yule jamaa aliacha kukata majani na kusogea kwa Sued.

ITAENDELEA........




TUPATIE NYOTA 5 KWENYE APP YETU KULE PLAY STORE NA KU COMMENT ILI TUPATE SUPPORT YAKO.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

CHOMBEZO: BINAMU 🔞 SEHEMU YA 11

KIJIJINI KWA BIBI SEHEMU YA 1-5

CHOMBEZO: MASSAGE ROOM🔞 SEHEMU YA 21