MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN SEHEMU YA 1
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 001
*Simulizi za series*
Jua lilinyanyuka na kuangaza ardhi ya Goshen: mojawapo ya tawala kubwa iliyopata kutokea mashariki ya mbali katika karne ya kumi baada ya kuzaliwa kwa kristo.
Ndege wake wakubwa wenye rangi za kuvutia waliamka wakaruka huku na kule wakitandaza sauti zao nyembamba. Sauti hizo marigoli zikawasili masikioni mwa malkia Sandarus na kumwamsha. Alikuwa amevalia nguo nyepesi za kulalia zilizokuwa zinaangaza kuonyesha mwili wake mchanga wa miaka ishirini na tano.
Kichwa chake chenye hekima kilikuwa kimefunikwa na nywele nyingi rangi ya kahawia. Miguu yake mirefu ila yenye nyama ilisimika ardhini na kusimamisha mwili wake mrefu mwembamba. Alah! Alikuwa mzuri haswa. Macho yake yalikuwa makubwa yaliyolegea. Mdomo wake ulikuwa mdogo ila hakika ukichanua kwa tabasamu ungekufanya uache shughuli yako na kumtazama.
Nyonga zake zilijiachanua na kukikimbia kiuno. Vidole vyake vilikuwa vyembamba virefu vyenye kucha bawabu. Tumbo lake flati na mapaja mekundu. Amini nakuambia siwezi kumaliza kuongelea uzuri wake kwani nikifanya hivyo tutajaza kitabu hiki.
Alipiga mihayo akanyoosha viungo vyake. Aliendea dirisha akafungua na kuangaza kutazama nje ya jengo lake kubwa la kifalme. Huko akaona makazi ya wananchi na wananachi wake wakiamka, wakikatiza na hata wakishughulika.
Alitabasamu akarejea kitandani kabla tu ya punde kijakazi wake kuingia akiwa kavalia gauni refu la kaki na kiremba kizito. Aliinama kumsalimu malkia kisha akamtazama na tabasamu.
“Malkia wangu, nimewasili. Nini wataka?”
“Hakuna ninachohitaji Zura.” Alisema Malkia Sandarus kwa sauti yake nyembamba ila yenye amri ndani yake.
Zura, kijakazi wa malkia, alikuwa ni mwanamama mzee wa miaka arobaini na tano. Si tu kwamba alikuwa ni kijakazi, bali pia alikuwa kama mama kwa Malkia huyo aliyempoteza mama yake punde tu alipozaliwa. Na kwa mujibu wa taratibu za kipindi hiko, Sandarus alipata mwanaume akiwa mdogo kabisa wa umri wa miaka mitano.
Alichukuliwa na mfalme wa Goshen, kwa jina Loop, kwa mujibu wa kumlelea ili aje kumuoa. Na kwa wakati wote huo, Sandarus akamjua Zura kama mama. Ni pale tu alipokuwa ndipo akapata kuujua kweli hizi chungu: hana mama, hampendi mwanaume aliyeozwa naye, baba yake hayupo tena hai, hana kaka wala dada, lakini pia pale alipo si nyumbani, nyumbani kwao ni kusini ya mbali kwenye utawala wa Maam.
Baba yake alikuwa mtu mkubwa kwenye hiyo tawala na kama mojawapo ya njia ya kuunganisha tawala hizi mbili: Goshen na Maam, babaye akamtoa akaolewe huko.
Tokea akiwa mtoto, Zura alimlea kama mwanaye. Lakini zaidi ya hapo alifanikiwa kumuandalia mazingira mazuri malkia huyo kuwa karibu sana na wananchi wake. Akiwa mtoto, alienda kuchota maji na hata kucheza na wanachi wa kawaida.
Hakuwa na majivuno wala malezi ya kunanga, matokeo yake watu wengi ndani ya tawala hiyo wakampenda na kufurahishwa naye.
“Ungependelea chakula gani mama?” Zura alimuuliza malkia akiwa ameinamisha uso wake chini. Malkia Sandarus alitabasamu akamjongea karibu na kumshika mabega.
“Unajua nini napendelea, mama.”
“Naitwa Zura, malkia.”
“Najua.”
“Ukiniita mama, nitashitakiwa. Nimeonywa sana juu ya hilo. Sina hadhi ya kuwa mama wa malkia.”
“Tafadhali. Siwezi kuacha kukuita mama. Na kama kuna yeyote atakayekufanya kitu basi atashughulika na mimi.”
Zura hakusema tena kitu. Amekuwa akisema hilo jambo la kuitwa mama kila siku na inaonekana anaongea na sikio la kufa. Aliufunga mdomo wake akafuata chakula akipendacho malkia wake: Aliporejea na kuhakikisha malkia wake anakula, aligeuza aondoke ila akaitwa pale tu alipofika mlangoni.
“Mfalme anaendeleaje?” Aliuliza Malkia Sandarus akila.
“Unamaanisha mumeo?” Zura aliuliza.
“Namaanisha mfalme.” Malkia Sandarus akajibu. Zura aliguna kwanza kisha akachukua hatua chache zilizomfikisha kitandani alipoketi na malkia wake.
“Malkia, inabidi ifikie mahali ukubali ya kwamba mfalme ni mumeo. Hakuna kitakachobadili hilo kamwe.”
“Sitaki kuongelea hayo mambo, mama.”
Hilo ndilo lilikuwa jibu la Malkia Sandarus kila alipoongea na Zura kumhusu mumewe – Mfalme Loop. Hakumpenda mwanaume huyo.
Matendo yake ya kumbaka kila siku kwanguvu lakini pia kumpiga mara kwa mara kulimfanya Malkia Sandarus amchukie mwanaume huyo zaidi. Ni kwakuwa tu aliwapenda watu wa Goshen ndiyo mana alikuwepo pale, ni kwakuwa tu watu wa Goshen walimpenda ndio mana alikuwa pale la sivyo angekuwa tayari ameshatoroka, kama kila siku anavyosema.
Baada ya kumaliza kula na kujiandaa kwa mavazi maridadi Malkia Sandarus aliongozana na Zura wakaenda kwenye kingo ya mto wa Boa wakiongozana na walinzi watano waliojibebelea kwenye farasi.
Huko walinzi walikaa kando kidogo kuwapisha wanawake hao kuteta na kutembea. Walisogea mbali zaidi na walinzi, Zura akamshika mkono Sandarus na kuhakikisha kwanza kama wapo mwenyewe. Ni kweli walikuwa wenyewe. Sasa akamnong’oneza:
“Kuna kitu nataka nikuambie.”
Malkia Sandarus aliogopa. Hakuwahi kumuona Zura katika hali hiyo na bila shaka sasa alitegemea kuna kitu makini anataka kuambiwa. Zura alitazama tena kushoto na kulia akarudia:
“Kuna kitu nataka nikuambie.”
“Sema.” Malkia Sandarus alisema kwa pupa. Sauti yake ililowa hofu. Alikuwa anaishiwa staha ya kungoja sasa. Zura alishusha pumzi ndefu, akasema:
“Kuna kitu niliambiwa nikupatie.”
“Kitu gani?”
“Mkufu. Baba yako kabla hajafariki alinihasa nikupatie mkufu huo. Lakini kwa siri sana, na haitakiwi yoyote aone wala kuuvaa kabisa.”
Malkia alikunja sura. Kuna kitu alihisi akipo sawa. Alijua baba yake amefariki tena kabla hata hajapata uwezo wa kumkumbuka kwa undani. Kwanini leo hii anapewa hiko kitu?
Na kwanini mkufu na si kingineko? Maswali hayo yalikuja upesi mno kichwani kwake. Aliyauliza Zura akamjibu kwa utulivu:
“Nimeshindwa kabisa kuendelea kutunza jambo hilo kifuani mwangu. Ila ujue kwamba wakati baba yako anafariki aliniita faragha akanipatia mkufu huo kwasababu aliniamini. Aliniambia hata mfalme asijue hilo. Aliniambia na kunielekeza mengi juu ya huo mkufu, lakini pia …” Hakumalizia. “Lakini nini?” Malkia aliwahi kuuliza.
Zura alitazama chini asiseme kitu. Alitazama tu maji ya mto yakitiririka. Kifuani mwake kuna jambo alikuwa anataka sema ila alikuwa anaogopa. Haikuwa na mantiki sasa kulificha jambo hilo ilhali ameshagusia jambo la mkufu, moyo wake ulimwambia.
Wakati akiyafikiria hayo Malkia alikuwa anamtazama kwa matamanio ya kutaka kusikia.
“Unatakiwa uvae mkufu huo baada tu ya mfalme kufa.” Alisema Zura.
“Kwanini?” Malkia Sandarus akauliza.
“Sijajua kwanini ila ndivyo baba yako alivyoniambia.”
Haikuleta maana kwanini mkufu huo una masharti hivyo. Hakuna aliyejua, hata Zura mwenyewe aliyekabidhiwa alikuwa ana ufahamu finyu juu ya hilo.
Waliondoka huko mtoni wakaelekea mpaka nyumbani kwa Zura, huko mkufu ukachopolewa toka kwenye kiboksi kidogo cheusi cha mbao, akakabidhiwa Malkia Sandarus. Mkufu huo ulipoketi kwenye kiganja cha mwanamke huyo, uling’aa kisha ukazima ghafla.
“Ndio huo!” Zura alisema.
Ghafla mlango ulifunguliwa akaingia mwanaume mnene mwenye ndevu na nywele nyingi. Alikuwa ni mume wa Zura. Mkufu ulifichwa haraka asipate kuuona. Alipomuona Malkia alipiga magoti akasalimu.
“Naweza nikaenda?” Malkia aliuliza akimtazama Zura.
“Ndio waweza kwenda, malkia wangu.”
Kabla hajaenda, akasema:
“Nitahitaji kukuona muda si mrefu.”
Aliondoka akaenda kuketi mwenyewe chumbani kwake. Alitazama mkufu ule aliopatiwa akiupekuapekua na maswali mengi yasiyo na majibu yakigonga kichwani. Mwishowe aliutia ndani ya kiboksi na kukiweka chini ya uvungu mwa kitanda.
Baada ya siku mbili, mfalme Loop alifariki dunia. Msiba wake ulivuma na wakuu wa tawala kadha wa kadha wakahudhuria. Alifariki akiwa na miaka mia moja kamili.
Msiba wake ulidumu kwa juma moja kisha baraza la wazee wa tawala la Goshen likaketi kwa ajili ya kuzungumza na kupanga juu ya nani ataendeleza utawala tangu mfalme akiwa hai hakufanikiwa kupata hata mtoto mmoja toka kwa wake zake wote wanne.
Kwenye majadiliano ya baraza hilo akateuliwa Mzee Fursa kusimamia tawala ya Goshen kwa muda wa takribani mwezi mmoja wakati mchakato wa kumpata mrithi ukifanyika kwa kukusanya maoni toka kwa wajumbe na pia wananchi.
Ndani ya muda huo wa mwezi, siku moja ikiwa ni katikati ya usiku mnene, Malkia Sandarus aliamka toka usingizini baada ya kusikia sauti ya kitu kikigonga mbao.
Alifungua macho yake akastaajabu kukuta chumba chake kikubwa chenye kila aina ya samani za ghali na za kupendeza kikiwa na mwanga mwekundu hafifu. Alifuatilia mwanga huo akagundua unatoka chini ya uvungu wake wa kitanda.
Alitaka kuita mlinzi aliyekuwa amesimama nje ya mlango, ila akasita. Alijibandua toka kitandani akachungulia chini ya kitanda, akaona mwanga huo watoka ndani ya kisanduku kile cheusi alichokabidhiwa na Zura.
Ilikuwa ni mkufu? Alijiuliza na nafsiye.
Alivuta kisanduku hicho akakifunua na kutazama. Kweli ilikuwa ni mkufu! Ulikuwa unawaka kama vile ulivyowaka kwa mara ya kwanza ulipotiwa mkononi mwake. Alibakia akiutazama mkufu huo na kujiuliza maswali kadhaa: kwanini unawaka? Kwanini alikabidhiwa tena kwa masharti?
Akiwa anaupekuapekua kwa kuugeuzageuza, pasipo kujua mwanga wa mkufu huo ukapenya chini ya mlango na kutua kwenye kiatu kikubwa cha mlinzi aliyekuwa amesimama huko nje.
Mlinzi alipata wasi akagonga mlango kuulizia usalama. Ila ajabu, mwanga wa mkufu ulijifinya na kupotea ghafla.
Malkia Sandarus aliurudisha mkufu huo ndani ya kisanduku kisha akajilaza. Usingizi haukumjia haraka kwasababu ya mawazo yaliyokuwa yamemtinda. Alitamani pakuche ili apate fursa ya kuulizana hilo jambo na Zura maana ndiye mtu pekee anayeweza kujadili naye juu ya mkufu huo.
Palikucha na alipoamka tu, alikutana na uso kwa uso na Zura. Alikuwa tayari ameshafika kwa ajili ya kufanya usafi na kusikiliza haja za malkia wake. Malkia alimueleza yale yote aliyopata kuyaona usiku, Zura akamkumbusha:
“Malkia wangu, uliambiwa uvae mkufu huo punde tu mfalme atakapokufa.”
“Na je nikiulizwa ni wapi nilipoutoa, nitasemaje?”
“Utalaghai mfalme alikuletea kama zawadi toka tawala za mbali.”
Malkia Sandarus alivaa mkufu huo, punde ukawaka na kuzima kama vile ulivyofanya kipindi cha kwanza kabisa. Hapo zikapita siku kadhaa na kukaribia kabisa siku ya kuwasilishwa maoni na mapendekezo ya wajumbe na wananchi juu ya nani atachukua utawala wa Goshen. .
.
.
.
.*** .
.
.
.
Katikati ya usiku mnene wa kuamkia siku ya mapendekezo na maoni, Malkia Sandarus alihisi joto kali kwenye kifua chake. Aliamka upesi kutazama akakuta kidani cha mkufu wake chawaka na kumetameta.
Alidhani ni kama siku zile, ila baada ya muda kidogo akagundua haikuwa kama siku zile kwani siku ile mkufu huo hakumuunguza na wala haukuwa wa moto kama siku hiyo. Haraka alivua akauweka mkononi. Ilimchukua muda mfupi tu akagundua kwamba kuna kitu.
Ndio.
Ukiachana na mwanga uliokuwa unamulika, kulikuwa kuna kitu ndani ya mwanga huo. Alitazama ukutani akaona picha ya mtu ndani ya huo mwanga. Alikuwa ni mwanaume mnene, mrefu mweusi.
Alitazama vema akagundua mwanaume huyo alikuwa ni mzee Fursa. Alikuwa anaongea na wazee watatu wa baraza na kandokando mwao walikuwepo wanajeshi watatu.
“Hatuwezi tukakubaliana na hili.” Sauti ya Fursa ilisikika toka mkufuni. Malkia Sandarus alisogeza masikio yake kwenye mkufu huku macho yake yakiangaza ukutani. “Mwanamke atatuongozaje?
Siwezi kabisa nikaheshimu maoni haya. Na hii ni kwa ajili ya Goshen. Endapo tukiruhusu akashika madaraka, basi lazima tutayumba na hakika Jayit muuaji atatuvamia na kuifanya hii tawala kuwa simulizi.”
Jayit ni mtawala wa Devonship. Tawala hiyo ipo upande wa magharibi ya mbali na tangu iundwe haijawahi kupatana na tawala ya Goshen hata kidogo. Chanzo cha chuki na uhasama wao ni vita iliyotokea huko miaka ya nyuma kwasababu ya kugombania ardhi ya makaburi.
Mtawala huyo wa Devonship alitaka ardhi hiyo kwa madai babu yake alizikwa hapo. Anahitaji ardhi hiyo hata kama kwa muda huo hakuwa tena mkazi wa Goshen. Hakuna aliyejua mpaka sasa kwanini anataka makaburi hayo, ila ndani ya roho yake alikuwa na kazi nayo kubwa na muhimu mno.
Kazi hiyo kwa miaka nenda rudi haijapata kutimia kwasababu tu ya kuhofia utawala wa Goshen chini ya familia ya Loop.
Ila kwa sasa familia hiyo imeenda baada ya mazishi, na haijaacha hata mtu wa kuendeleza utawala huo uliokuwa na mahusiano makubwa na tawala za karibu. Sasa Jayit anaona hiyo ni fursa marigoli kupata anachokitimiza. Hiyo ndio fursa adhimu ya kutimiza haja zake:
Kupata ardhi ya makaburi!
Malkia Sandarus alishika mdomo wake kwa mshangao akitazama ukutani. Hakuamini alichokuwa anakiona. Hakuamini kama mzee Fursa anaweza akapanga tukio kama lile la kupuuza mapendekezo na maoni ya wananchi. Na si tu kwamba ameishia hapo ila sasa alikuwa ameagiza wanajeshi wale watatu waje kummaliza!
Kwa muda kidogo Malkia hakuamini kile alichokuwa anakiona. Kwa namna moja ama nyingine alihisi analaghaiwa na ule mkufu ambao umepanga kumkosanisha na watu wake. Ila baada ya muda mfupi alijikuta ananza kusadiki.
Alisikia sauti ya mwanajeshi ikilalamika kwa maumivu mlangoni kisha akasikia kishindo cha mtu akidondoka. Ghafla mwanga wa mkufu ulizima na kukawa giza. Na sasa mlango wake ukawa unapigwa kwanguvu ukilengwa kuvunjwa! Moyo wake ulitatuka. Ni haraka akajikuta anapata joto kali mwilini la kutosha kabisa kumvujisha jasho.
.
.
.
ITAENDELEA........
TUPATIE NYOTA 5 KWENYE APP YETU KULE PLAY STORE NA KU COMMENT ILI TUPATE SUPPORT YAKO.
Maoni
Chapisha Maoni